Ticker

6/recent/ticker-posts

zinduka,, hizi ni njia za mafanikio

MTU anafanikiwa kikweli kwa kupata njia bora kabisa ya maisha ambayo inatokana na kufuata viwango vya Mungu na kuishi kupatana na kusudi la Mungu kwa wanadamu. Biblia inasema kwamba mtu anayeishi maisha ya aina hiyo “atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.”Zaburi 1:3.
Naam, ingawa sisi si wakamilifu na tunafanya makosa, tunaweza kufanikiwa maishani! Je, hilo linakuvutia? Ikiwa ndivyo, basi kanuni sita zinazofuata za Biblia zinaweza kukusaidia ufikie lengo hilo na hivyo kuthibitisha waziwazi kwamba kwa kweli mafundisho ya Biblia ni hekima inayotoka kwa Mungu.—Yakobo 3:17.
1 Uwe na Maoni Yanayofaa Kuhusu Pesa
“Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine . . . wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”(1 Timotheo 6:10) Ona kwamba tatizo si pesa, kwa kuwa sisi sote tunahitaji pesa ili kujitunza na kutunza familia zetu. Tatizo ni kupenda pesa. Kwa kweli, upendo huo hufanya pesa ziwe bwana, au mungu.
Kama tulivyoona katika makala ya kwanza ya mfululizo huu, watu ambao hukimbizana na utajiri ili wapate mafanikio, kwa kweli wanafuatilia upepo. Mbali na kutamaushwa wanapatwa na maumivu mengi. Kwa mfano, katika jitihada zao za kutafuta mali nyingi, mara nyingi watu hupuuza uhusiano wao wa familia na marafiki. Wengine hukosa usingizi, si kwa sababu ya kazi tu, bali pia kwa sababu ya wasiwasi. “Usingizi wa kibarua ni mtamu, awe ameshiba au amekula kidogo tu. Lakini usingizi wa tajiri ni wa wasiwasi daima, maana ziada ya mali yake humsumbua usiku kucha,” inasema Mhubiri 5:12.—Biblia Habari Njema.
Zaidi ya kuwa bwana mkatili, pesa ni bwana mdanganyifu pia. Yesu Kristo alizungumza kuhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19) Hilo linamaanisha kwamba utajiri humwahidi mtu kwamba utampa furaha, lakini haufanyi hivyo. Badala yake unamfanya mtu atamani utajiri zaidi. “Anayependa fedha hatatosheka na fedha,” inasema Mhubiri 5:10.
Kwa ufupi, mtu anayependa pesa anajiumiza tu. Anavunjika moyo, anakatishwa tamaa, au hata kujihusisha katika uhalifu. (Methali 28:20) Ukarimu, kuwa tayari kusamehe, usafi wa maadili, upendo, na uhusiano mzuri pamoja na Mungu, ni mambo yanayoleta furaha na mafanikio.
2 Sitawisha Roho ya Ukarimu
“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ingawa kuwapa watu vitu mara kwa mara kunaweza kumfanya mtu awe na furaha ya muda, roho ya ukarimu inaweza kumfanya awe na furaha ya kudumu. Ni kweli kwamba kuna njia mbalimbali za kuonyesha ukarimu. Mojawapo ya njia bora na inayothaminiwa sana ni kutenga wakati ili kuwa pamoja na watu na kufanya mambo nao.
Baada ya kupitia uchunguzi mwingi kuhusu furaha, afya, na kutokuwa na ubinafsi, mchunguzi Stephen G. Post alisema kwamba kutokuwa na ubinafsi na kuwasaidia wengine kunahusianishwa na maisha marefu, afya nzuri kimwili na kiakili, kutia ndani kupunguza kushuka moyo.
Isitoshe, watu wanaowapa watu vitu kwa ukawaida hawapungukiwi na chochote maishani kwa sababu tu ya kuwa wakarimu. Methali 11:25 inasema hivi: “Mtu mkarimu atafanikishwa, amnyweshaye mwingine maji naye atanyweshwa.” (BHN) Kupatana na maneno hayo, watu ambao ni wakarimu kutoka moyoni, ambao hawawapi watu vitu wakitarajia kulipwa, wanathaminiwa na kupendwa na Mungu.—Waebrania 13:16.
3 Samehe kwa Hiari
“Endeleeni . . . kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”(Wakolosai 3:13) Siku hizi, watu hawako tayari kusamehe; wao hulipiza kisasi badala ya kuonyesha rehema. Matokeo ni nini? Wanapotukanwa wanatukana, nao hulipiza jeuri kwa jeuri.
Mambo hayaishii hapo tu. Ripoti moja katika gazeti The Gazette la Montreal, Kanada inasema kwamba “katika uchunguzi uliofanyiwa watu zaidi ya 4,600 wenye umri ya kati ya miaka 18 hadi 30,” wachunguzi “waligundua kwamba uhasama, kukata tamaa, na kutokuwa na fadhili” hufanya mapafu yawe mabovu. Kwa kweli, mambo hayo yanaweza kufanya mapafu ya mtu kuwa mabovu zaidi kuliko ya mvutaji wa sigara! Bila shaka, kusamehe hakufanyi iwe rahisi kushughulika na wengine tu bali pia kunafaidi afya yetu!
Unawezaje kusamehe zaidi? Anza kwa kujichunguza kwa unyoofu. Je, nyakati nyingine huwakasirishi watu? Unafurahi wanapokusamehe? Kwa hiyo, mbona usiwaonyeshe wengine rehema? (Mathayo 18:21-35) Pia ni muhimu kujizuia. “Hesabu moja hadi kumi” au tafuta wakati ili utulize hasira. Tambua kwamba kujizuia si udhaifu. “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu,” inasema Methali 16:32. Maneno “ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu” yanaonyesha mtu amefanikiwa kikweli, sivyo?
4 Ishi Kulingana na Viwango vya Mungu
“Amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae.” (Zaburi 19:8) Kwa ufupi, viwango vya Mungu vinatufaidi, kimwili, kiakili, na kihisia. Vinatulinda dhidi ya mazoea yenye kudhuru kama vile, kutumia dawa za kulevya, kulewa, ukosefu wa maadili, na kutazama ponografia (picha au habari za ngono). (2 Wakorintho 7:1; Wakolosai 3:5) Huenda mazoea hayo yakatokeza madhara mabaya kama vile uhalifu, umaskini, kutoaminiana, kuvunjika kwa familia, matatizo ya kiakili na kihisia, magonjwa, na kifo cha mapema.
Kwa upande mwingine, wale wanaoishi kulingana na viwango vya Mungu wanakuwa na mahusiano mazuri, pia wanajiheshimu, na kuwa na amani ya akili. Katika Isaya 48:17, 18, Mungu anasema kwamba yeye ndiye “anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” Kisha anaongeza hivi: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” Ndiyo, Muumba wetu anatutakia maisha bora zaidi. Anataka ‘tuende katika njia’ ya mafanikio ya kweli.
5 Onyesha Upendo Usio na Ubinafsi
“Upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Je, unaweza kuwazia maisha yasiyo na upendo? Yangekuwa maisha yasiyo na maana kama nini! “Ikiwa . . . sina upendo [kwa wengine], mimi si kitu. . . . Sipati faida hata kidogo,” akaandika Paulo, mtume Mkristo aliyeongozwa na roho ya Mungu.—1 Wakorintho 13:2, 3.
Upendo unaotajwa hapa si ule wa kimahaba ambao una mahali pake panapofaa. Badala yake ni upendo unaodumu ambao unaongozwa na kanuni za Mungu.* (Mathayo 22:37-39) Isitoshe, mtu haonyeshwi tu upendo huo bali anauonyesha kwa matendo. Paulo aliendelea kusema kwamba upendo huo ni wenye subira na pia fadhili. Hauna wivu, haujigambi, au kujivuna. Hutafuta faida za wengine, na hauchokozeki kwa urahisi bali ni wenye kusamehe. Upendo kama huo hujenga. Pia, unatusaidia tuwe na uhusiano mzuri na wengine hasa washiriki wa familia.—1 Wakorintho 13:4-8.
Kwa wazazi, upendo unamaanisha kuwa na hisia nyororo kuwaelekea watoto wao na kuwapa mwongozo ulio wazi unaotegemea Biblia kuhusu maadili na tabia nyingine. Watoto wanaolelewa katika mazingira kama hayo hujihisi salama, wanapendwa, na kuthaminiwa wakiwa sehemu ya familia iliyo imara.—Waefeso 5:33–6:4; Wakolosai 3:20.
Jack, anayeishi Marekani, ni kijana aliyelelewa katika familia iliyofuata kanuni za Biblia. Baada ya kuondoka nyumbani, Jack aliwaandikia wazazi wake barua. Sehemu ya barua hiyo ilisema hivi: “Jambo moja ambalo nimejitahidi kufanya ni kufuata agizo [la Biblia] linalosema: ‘Mheshimu baba yako na mama yako . . . ili mambo yakuendee vema.’ (Kumbukumbu la Torati 5:16) Mambo yameniendea vema. Na sasa ninathamini kwamba imekuwa hivyo kwa sababu mlijitahidi kunilea kwa upendo. Asanteni sana kwa kunitegemeza na kwa jitihada zenu nyingi za kunilea.” Kama wewe ni mzazi, ungehisije kama ungepokea barua kama hiyo? Je, hungejawa na shangwe moyoni?
Pia, upendo unaotegemea kanuni ‘unashangilia pamoja na kweli,’ yaani, kweli kumhusu Mungu inayopatikana katika Biblia. (1 Wakorintho 13:6; Yohana 17:17) Ili kufafanua, fikiria mfano huu: Wenzi walio na matatizo katika ndoa yao wanaamua kusoma pamoja maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Marko 10:9: “Kwa hiyo kile ambacho Mungu ameunganisha [katika ndoa] mtu yeyote asikitenganishe.” Sasa, lazima wajichunguze mioyo yao. Je, kweli ‘wanashangilia pamoja na kweli za Biblia’? Je, wataiona na kuitendea ndoa kama kitu kitakatifu, kama vile Mungu anavyoiona? Je, wako tayari kujitahidi kutatua matatizo yao kwa upendo? Kwa kufanya hivyo wanaweza kufanya ndoa yao ifanikiwe, na wanaweza kushangilia matokeo mazuri ya jitihada zao.
6 Tambua Uhitaji Wako wa Kiroho
“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Tofauti na wanyama, wanadamu wana uwezo wa kuthamini mambo ya kiroho. Kwa sababu hiyo, sisi hujiuliza maswali kama haya, Ni nini kusudi la uhai? Je, kuna Muumba? Ni nini hutupata tunapokufa? Wakati ujao utakuwaje?
Ulimwenguni pote, mamilioni ya watu wanyoofu wametambua kwamba Biblia inajibu maswali hayo. Kwa mfano, swali la mwisho linahusiana na kusudi la Mungu kwa wanadamu. Kusudi hilo ni nini? Ni kwamba dunia iwe paradiso inayokaliwa na watu wanaompenda Mungu na viwango vyake. Zaburi 37:29 inasema: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”
Ni wazi kwamba Muumba wetu anataka tufanikiwe kwa muda mrefu zaidi kuliko miaka 70 au 80 tu. Anataka tufanikiwe milele! Kwa hiyo, sasa ndio wakati wako wa kujifunza kuhusu Muumba wako. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Unapoendelea kupata ujuzi huo na kuutumia maishani, utagundua kwamba “baraka ya Yehova . . . ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.
[Maelezo ya Chini]
Karibu kila mahali ambapo neno “upendo” linatumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo au “Agano Jipya” linatafsiriwa kutoka kwa neno la Kigiriki a·gaʹpe. A·gaʹpe ni upendo wa maadili unaochochewa na kanuni, wajibu, au kutaka kufanya jambo unalopaswa kufanya. Hata hivyo, a·gaʹpe si upendo usio na hisia bali unaweza kuwa wenye kina na mchangamfu.—1 Petro 1:22.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
MAMBO ZAIDI YANAYOLETA MAFANIKIO
▪ Mwogope Mungu kwa njia inayofaa. “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima.”—Methali 9:10.
▪ Chagua marafiki kwa hekima. “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.
▪ Epuka kunywa au kula kupita kiasi. “Mlevi na mlafi watakuwa maskini.”—Methali 23:21.
▪ Usilipize kisasi. “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.”—Waroma 12:17.
▪ Fanya kazi kwa bidii. “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, basi na asile chakula.”—2 Wathesalonike 3:10.
▪ Fuata ile Kanuni Bora. “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.
▪ Dhibiti ulimi wako. “Yeye ambaye anapenda uzima na kuona siku zilizo njema, na auzuie ulimi wake kutokana na yaliyo mabaya.”—1 Petro 3:10.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
UPENDO NI DAWA NZURI
Dean Ornish, ambaye ni daktari na pia mwandishi anaandika hivi: “Upendo na mahusiano ya karibu ni sababu kuu zinazoweza kutufanya tuwe wagonjwa au tuwe wenye afya, tuhuzunike au tuwe wenye furaha, tuteseke au tupone. Ikiwa dawa mpya ingekuwa na matokeo kama hayo, karibu kila daktari nchini angeipendekeza kwa wagonjwa wake. Ingekuwa kinyume cha sheria za kitiba kukataa kumwandikia mgonjwa dawa hiyo.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
ALIYEKATA TAMAA AFANIKIWA
Vita vilipoanza katika nchi yake, Milanko, anayeishi huko Balkani, alijiunga na jeshi. Kwa sababu ya ujasiri wake, alipewa jina la utani Rambo ambalo ni jina la shujaa katika sinema moja ya jeuri. Hata hivyo, baada ya muda Milanko alikatishwa tamaa na ufisadi na unafiki alioona jeshini. Anaandika hivi: “Kwa sababu hiyo nilijihusisha na mambo mengi maovu kama vile kutumia vileo, sigara, dawa za kulevya, kucheza kamari, na ukosefu wa maadili. Maisha yangu yalikuwa mabaya na sikujua jinsi ya kuyaboresha.”
Katika kipindi hicho cha msukosuko maishani mwake, Milanko alianza kusoma Biblia. Baadaye, alipokuwa akimtembelea mtu wa ukoo, aliona gazeti Mnara wa Mlinzilinalochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Alifurahia mambo aliyosoma na muda si muda akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Kweli za Biblia zilimfanya awe na furaha na mafanikio ya kweli. Anasema hivi: “Zilinipa nguvu mpya, niliacha matendo yangu yote maovu, nikawa mtu mpya, na nikabatizwa kama Shahidi wa Yehova. Watu walionijua zamani hawaniiti Rambo tena, bali Sungura, jina langu la utotoni kwa sababu ya upole wangu.”

Post a Comment

0 Comments